BREAKING NEWS

Gallery

neno
Showing posts with label neno. Show all posts
Showing posts with label neno. Show all posts

Tuesday, 11 August 2015

NDEGE TAI JIFUNZE KWAKE



NDEGE TAI JIFUNZE KWAKE
Ninampenda Yesu's photo.

Tai huwa hapambani na nyoka juu ya ardhi. Yeye humnyakuwa na kwenda naye juu sana angani, na hivyo kubadilisha uwanja wa mapambano, halafu humshambulia na kumwachia adondoke chini ardhini. Nyoka huwa hana 'stamina', hana nguvu, wala ‘balance’ akiwa hewani. Huwa mdhaifu, mwepesi kudhurika na asiye na uwezo wa kufanya chochote tofauti na awapo juu ya ardhi ambapo huwa ni hatari, mjanja na mwenye nguvu.
Nawe kama mwana wa Mungu, unapokutana na adui zako na kupigwa vita hamishia mapambano yako katika ulimwengu wa Kiroho ambapo Mungu huchukua nafasi. Usipambane na changamoto zako katika ulimwengu wa kimwili; Jifunze kwa Tai na kubadili uwanja wa mapambano kama yeye. Hapo ndipo utakuwa na uhakika wa ushindi usio wa upinzani. Omba na umwachie Mungu ingilie kati.
Lakini unapopambana katika ulimwengu wa Kiroho kumbuka; kutegemea nguvu za Mungu, sio nguvu zako (2 Wakorintho 10:3) kwa sababu kushinda vita hii hauhitaji nguvu za kimwili, bali akili ya kiroho, kukemea kwa jina la Yesu (Matendo Ya Mitume 19:13-17), kukaa ndani ya Yesu na kujikinga kwa kuvaa silaha zote za Mungu (Yohana 15:7, Warumi 13:12-14 na Waefeso 6:10-18), kupigana vita kwa upanga wa roho ambao ni Neno la Mungu, na mwisho kukumbuka kwamba, unapopigana vita vya kiroho na Shetani na mapepo yake, sio kila dhambi au taabu ni pepo ambalo linahitaji kukemewa.
Ngoja nikupe simulizi moja niliyowahi kusimuliwa na mdogo wangu Loveness Mlay; Kuna siku wanamaombi walikuwa wakimwombea binti mmoja aliyekuwa akipiga kelele kama aliyepagawa na pepo; kwa muda mrefu walimwombea na kukemea lakini mapepo hayo hayakutoka, Mchungaji alipokuja akawanong’oneza kuwa anaona huyo binti hana pepo kwa hiyo watoke nje ya chumba na wamwache pekeyake kwa muda… Baada ya muda kidogo kupita binti akiwa ameachwa pekeyake akaacha kupiga zile kelele kama wafanyavyo wapunga pepo, kukawa kimya; nao walipochungulia wakamuona binti akiangaza macho ili kuona kama kuna mtu karibu anamwangalia; alipoona hakuna mtu akainuka na kuondoka zake. Kwa hiyo umwonapo mtu akipiga kelele kama wapunga pepo wafanyavyo mtazame kwa macho ya rohoni kwani wengine hujifanyisha na unapokemea kelele zao unatumia nguvu za Mungu vibaya.
Ila pia unapoona kama vita ni ngumu kwako kumbuka vita si yako bali ni ya Mungu, (2 Mambo Ya Nyakati 20:14-15) kwa hiyo yakupasa upigane kwa imani!
Ninamwomba Mungu akusaidie kufanikiwa kwa hili katika Jina la Yesu Kristo!

MAOMBI NI VITA! - MWAKASEGE


"Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho" EFE 6:12.

Ndugu yangu, Paulo anatueleza jambo zito sana katika waraka wake huu. Paulo anatufundisha kubeba silaha zote za kupigana na adui ili tuweze kusimama kwa ushindi katika hivi vita. Pamoja na silaha zote anamalizia katika mstari wa kumi na nane kwa kusema kwamba "kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo ".!
Anatuambia kwamba kupigana kwetu huku ni kwa njia ya maombi! Kimahesabu, vita vyetu hivi tunavipiga kwa kutumia maombi. Vita hivi vya kiroho tunavipiga kwa kutumia maombi. Maombi ni silaha kubwa katika vita hivi. Ukiangalia silaha zote ambazo anazitaja (1. Kweli 2. Haki (Maisha safi yenye utii) 3. Utayari ktk huduma 4. Imani 5. Wokovu (Uhakika wa mahusiano ya mtu binafsi na Mungu) 6. Upanga wa Roho ambao Neno la Mungu ) Silaha kuu yenye kubeba silaha zote hivi ni maombi! "kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho".
Ndugu, kila siku unapaswa kukaa mkao wa kivita. Paulo anamuonyesha adui kama mtaalamu wa kupanga vita hivi. Ndo maana Paulo asema ktk mstari wa kumi na moja "Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani". Shetani ni mwenye hila kila wakati. Katika kazi zako ataweka hila, katika huduma yako ataweka hila. Katika kanisa lako ataweka hila. Katika uchumi wako ataweka hila. Kila kutaka kwako kumjua Mungu ataweka hila. Basi Paulo asema Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Basi acha kulala mtumishi. Simama tuvipige hivi vita. Kuna watu wanajiona hawana huduma katika kanisa. Huduma hii ya ukamanda wa maombi nafasi hii inakusubiri. Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Chukua hatua. Tumia mbinu zote za kivita vya kiroho tuweze kupambana na adui. 
Tuungane pamoja katika vita hii pia kwa ku-like page yetu tushirikiane katika kuvipiga vita hivi katika jina la Yesu na damu ya mwanakondoo.


Kama una jambo lolote/ una ushuhuda na unatamani tuwafahamishe na wengine basi usisite kuwasiliana nasi. Tuandikie kupitia:ushuhudainjili@gmail.com 

Usiache kutufuatilia kupitia facebook na twitter
Roho Mtakatifu akubariki.
--------------------------------------------

Mjue sana Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo mema yatakavyokujia